Na Theresia Mwami TEMESA Songea
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa ufundi na Umeme – TEMESA Dkt. Mussa Mgwatu, leo ametembelea na kukagua karakana ya TEMESA iliyopo Songea Mkoani Ruvuma na kumuagiza Meneja wake, Mhandisi Elisha Mulyila kuhakikisha Mashine zote zilizomo kwenye karakana ya vyuma zinafanyiwa ukarabati.
Dkt Mgwatu ameongeza kuwa ukarabati wa mashine hizo uzingatie ubora na utumie wataalamu wa ndani ya nchi ili kuwajenge uwezo wataalamu hao katika utengenezaji na ukarabati wa mashine mbalimbali.
Pia Dkt. Mgwatu alimuagiza Meneja huyo kuhakikisha kuwa kituo kinaibua kazi mbali mbali za utengenezaji vipuri kwa kutumia karakana ya uchongaji vyuma iliyopo kituoni hapo, kwani karakana hiyo inauwezo mkubwa wa kuweza kutosheleza mahitaji ya soko la uchongaji vyuma mkoani humo.
Kwa upande wake Meneja wa TEMESA Songea Mhandisi Elisha Mulyila alimuakikishia Mtendaji Mkuu huyo kuwa agizo lake litafanyiwa kazi kwa kuanza ukarabati wa mashine na vitendea kazi mara moja ili kuendelea na majukumu yao ya kila siku ya kuhudima vifaa muhimu hasa magari ya Serikali na Taasisi nyingine.
Mtendaji Mkuu wa TEMESA Dkt. Mussa Mgwatu yupo katika ziara ya kikazi kutembelea vituo vya TEMESA vilivyopo nyanda za juu Kusini ili kubaini changamoto mbali mbali zilizo kwenye vituo hivyo na kuzitafutia ufumbuzi.